1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashirika ya kijamii yaonya huenda udikteta ukarejea Kenya

Wakio Mbogho12 Oktoba 2017

Baadhi ya mashirika ya kijamii yanaonya kuwa Kenya huenda inarejelea uongozi wa kidikteta kufuatia kile wanachokiita kugandamizwa kwa taasisi muhimu na serikali ya Jubilee

https://p.dw.com/p/2li4t
Kenia Präsidentschaftswahl Proteste in Nairobi
Picha: Reuters/T. Mukoya

Baadhi ya mashirika ya kijamii yanaonya kuwa Kenya huenda inarejelea uongozi wa kidikteta kufuatia kile wanachokiita kugandamizwa kwa taasisi muhimu na serikali ya Jubilee. Mashirika haya yanaambatanisha matukio ya hivi karibuni kuelekea uchaguzi wa urais nchini ambapo viongozi wa kijamii, makanisa na vyombo vya habari vimeonekana kuegemea upande wa chama cha Jubilee, wakisema kuwa hali hiyo tayari ilikuwa imemnyima kiongozi wa upinzani, Raila Odinga, ushindi katika uchaguzi huo.

Mgawanyiko wa maoni

Maoni yamegawanyika kuhusu kile kinachomaanishwa na uamuzi wa kiongozi wa upinzani, Raila Odinga, wa kujitoa katika uchaguzi wa urais wa tarehe 26 mwezi huu wa Oktoba. Rais Uhuru Kenyata na wafusasi wake wameshikilia kuwa kura lazima ifanyike tarehe hiyo, jambo wanalolipinga wafuasi wa Raila Odinga.

Rais Uhuru Kenyatta akiwapungia mkono wafuasi wake mtaa wa Umoja Nairobi
Rais Uhuru Kenyatta akiwapungia mkono wafuasi wake mtaa wa Umoja NairobiPicha: Getty Images/AFP/T. Karumba

Masese Kemunche ambaye ni mratibu katika shirika la kijamii la CEDGG anaunga mkono hatua ya Raila akiitaja kama haki yake ya kikatiba. Aidha anahoji uwezekano wa uchaguzi huru na wa haki akisema chama cha jubilee tayari kilikuwa kimeweka mikakati kila upande kuhakikisha Raila hatashinda uchaguzi huo.

Unyamavu wa mashirika ya kijamii

Masese anayashutumu mashirika ya kijamii, makanisa na wanahabari nchini kwa kukosa kuangazia swala hili kikweli akisema serikali iliyopo imekandamiza taasisi hizi kiasi kwamba haziwezi kutoa mwongozo huru. Ametaja kuwa hata wataalamu kama mawakili wanajihusisha na chama cha Jubilee kwa lengo la kujipatia ukubwa. Kulingana na masese hizi ni ishara za kidikteta zinazotoshia uhuru wa taifa hili.

Ni swala linaloibuliwa pia na baraza la wazee wa jamii zilizoko eneo la Bonde la Ufa mbao wamewataka viongozi wa kanisa kutochukua misimamo ya kisiasa kufuatia hali ya kisiasa inavyojiri. Wamesema kuwa sawa na majaji na mahakimu, viongozi wa kanisa wana jukumu la kusimama wima na kutoa mweleko kwa wananchi.

Raila Odinga, kiongozi wa muungano wa upinzani NASA
Raila Odinga, kiongozi wa muungano wa upinzani NASAPicha: Reuters/B. Ratner

Maandamano yapigwa marufuku Nairobi, Mombasa na Kisumu

Masese Kemunche analitaka shirika la mawakili nchini, LSK, kutoa utafsiri kamili wa hatua hii ya Raila Odinga kuhusiana na kile inchomaanisha kwa uchaguzi wa Oktoba tarehe 26. Hatua hii, Masese anasema, itasitisha taharuki inayoibuliwa na mipango ya chama cha jubilee kubadilisha baadhi ya sheria zinazoonekana kuwa.

Kando na hayo, kaimu waziri wa usalama wa ndani, Fred Matiang'I ametangaza kupiga marufuku ya maandamano katika mjini mikuu akihusisha maandamano hayo na uharibifu wa mali katika miji hiyo. Itazingatiwa kuwa muungano wa upinzani nchini, NASA, ulikuwa umetoa mwongozo kwa wafuasi wake kuanza maandamano ya kila siku kuanzia kesho ili kushinikiza mageuzi katika tume huru ya uchaguzi nchini, IEBC.

 

Mwandishi: Wakio Mbogho/DW Nakuru

Mhariri: Mohammed Khelef