1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mhariri wa gazeti ayatuhumu makanisa ya Ujerumani

Sylvia Mwehozi
28 Desemba 2017

Mhariri wa moja ya magazeti yanayoongoza hapa Ujerumani ametawala mitandao ya kijamii baada ya kutoa kauli ya kutuhumu mahubiri ya Krismasi kwamba yalikuwa na upendeleo wa siasa za mrengo wa kushoto.

https://p.dw.com/p/2q2JP
Ulf Poschardt, stellvertretender Welt-Chefredakteur
Picha: picture alliance/dpa/P. Zinken

Mhariri mkuu wa gazeti la Die Welt, mojawapo ya magazeti yanayoongoza nchini Ujerumani na lenye mtazamo wa kihafidhina, amechochea mjadala katika mitandao ya kijamii wakati wa Krismasi baada ya kulalamika kwamba mahubiri yalikuwa ya upendeleo kwa mirengo ya kushoto katika misa ya usiku ya Krismasi.

Ulf Poschardt aliandika kupitia ukurasa wake wa twitter katika usiku wa mkesha wa Krismasi kwamba "Nani anaweza kwenda ibada ya usiku kwa hiari ikiwa mwisho wa ibada atajihisi kwamba ametumia siku yake na Jusor au tawi la vijana wa kijani?", akimaanisha matawi ya vijana ya vyama vya Social Democratic SPD na kile cha kijani, ambayo yote yanawakilisha mrengo wa kushoto wa vyama vyao.

Kauli yake ilikuja siku chache baada ya kiongozi wa chama siasa za mrengo mkali wa kulia cha AfD, Alice Wiedel kutoa malalamiko sawa kwa jarida la Focus akisema kwamba makanisa yameingiliwa na siasa.

Deutschland Kirche Kopten feiern Weihnachten in Düsseldorf
Padri akiongoza ibada mjini DusseldorfPicha: dapd

Haikuwa wazi ni ibada ipi ambayo mhariri wa gazeti la Die Welt alihudhuria au ikiwa alikuwa anamaanisha ibada moja tu , lakini ujumbe wa Krismasi wa viongozi wengi wa makanisa ya Ujerumani uliotolewa ulihusu wito wa umoja kwa wakimbizi, kupiga vita biashara ya Krismasi na kuendekeza anasa, ambavyo vyote kwa hakika vilikuwa vikiwatia hasira wafuasi wa chama kinachopigania biashara cha Free Democratic FDP, chama ambacho Poschardt aliwahi kusema ni mfuasi wake.

Kauli ya mhariri huyo katika ukurasa wake wa twitter iliamsha mjadala, wanasiasa kadhaa wa SPD na wale wa chama cha kijani nao walimjibu kupitia kurasa za Twitter. Mwenyekiti wa chama cha kijani Simone Peter alimjibu kwamba, "basi nitaenda tena katika ibada ya usiku. Inaonekana ni nzuri. Na tunahitaji uingiliaji kati zaidi kuliko wakati wowote na ukosefu wa usawa, kutengwa na mgogoro wa hali ya hewa".

Ricarda Lang, msemaji wa tawi la vijana la chama cha the Green, aliliambia gazeti la Frankfurter Allgemeine Zeitung siku ya Krismasi kwamba suala la kuzungumzia utu na mshikamano lilionekana kumkera mhariri huyo akiongeza kwamba hilo ni jukumu la jamii nzima.

Deutschland Sondierungsgespräche in Berlin - Simone Peter
Mwenyekiti wa chama cha kijani Simone PeterPicha: picture-alliance/dpa/K. Nietfeld

Msemaji wa shirika la kanisa la Kiprotestanti la Ujerumani EKD aliyatupilia mbali madai hayo ya Poschardt. Aliiambia DW  kwa njia ya barua pepe kuwa "taswira hiyo ya kupotoshwa haionyeshi  ukweli wa  maelfu ya mahubiri ya Krismasi kote Ujerumani. Haikuelewa haki ya kiroho ya kauli ya kanisa juu a masuala ya siasa. Mtu aliye mwaminifu wakati mwingine ni lazima awe na siasa."

Msemaji huyo aliendelea kusema kuwa ukweli ni kwamba mahubiri ya Krismasi ya mwaka 2017 yalikuwa tofauti na ukweli wa makanisa mawili makubwa katika nchi. ''Mimi mwenyewe niliona mahuiri ya Krismasi yaliyozungumzia kumbukumbu ya maadhimish ya mageuzi ya  ushawishi wa Martin Luther juu yatamaduni zetu za Krismasi'', aliongeza.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/dw

Mhariri: Daniel Gakuba