1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uhaba wa maji Marsabit Kenya wawatia wakaazi wasiwasi

Michael Kwena14 Januari 2019

Wakaazi wa kijiji cha Parkishon jimbo la Marsabit wakabiliwa na hofu ya kuathiriwa na mripuko wa magonjwa kufuatia uhaba wa maji. Wanaitaka wizara ya maji nchini humo kuwapa msaada wa dharura wa maji.

https://p.dw.com/p/3BX0L
Wassermangel in Marsabit, Kenia
Picha: Wassermangel , Wasser, Dürre, Trockenheit, Afrika, Marsabit, Kenia

Wakaazi wa kijiji kimoja katika jimbo la Marsabit nchini Kenya wanakabiliwa na hofu wa mripuko wa magonjwa kutokana na uhaba wa maji safi na salama. Wanailaumu serikali ya jimbo hilo kwa kuwatenga licha ya uhaba wa maji kuendelea kuwa tatizo kwa zaidi ya miaka 20 sasa jimboni humo. Wakaazi hao sasa wanaitaka wizara ya maji nchini humo kuwapa msaada wa dharura wa maji.

Kilio cha mama Sara Kasulah akieleza fedheha yake kutokana na ukosefu wa maji katika kijiji cha Parkishon ilioko eneo bunge la Saku jimboni Marsabit kinaeleza waziwazi masaibu yanayowakumba wakaazi wa eneo hili.  "Sisi tulipigia serikali kura lakini serikali yenyewe haioni shida yetu. Watoto hawaendi shule kutokana na ukosefu wa maji na hata wakienda shule, hatuwezi kuwapikia,hatuna maji”

Kijiji hiki chenye zaidi ya wakaazi 300,kinakabiliwa na mripuko wa ugonjwa wa kipindupindu kutokana na uhaba wa maji.

Kulingana naye,uhaba wa maji huwalazimisha kutembea kwa zaidi ya kilomita 10 kutafuta huduma hiyo adimu hapa jimboni.

Mama sarah anasema kuwa,mifugo wao pia wamo katika hatari ya kuangamia kutokana na ukosefu wa maji ya kuwanywesha.

Wafugaji wanasafiri kilomita kadhaa kufikia bwawa hili lenye maji
Wafugaji wanasafiri kilomita kadhaa kufikia bwawa hili lenye majiPicha: Wassermangel , Wasser, Dürre, Trockenheit, Afrika, Marsabit, Kenia

"Binadamu hali yake ni maji na kama hakuna maji,basi hakuna pia maisha.Mifugo hawana maji na sisi pia tunalazimika kunywa maji machafu.Tunachanganya jivu na maji kisha tunapikia,ni shida tupu”

Wanakijiji wanahisi kutengwa katika miradi ya usambazaji maji mashinani na serikali ya jimbo.

Leyado Lesipan ambaye ni mmoja wa wazee wa kijiji hiki anasema: " viongozi wote wa utawala wako hapa, lakini hakuna walichotusaidia kwenye shida hii ya maji”

Hata hivyo,gavana wa jimbo hili Muhammud Ali ameahidi kulishugulikia tatizo hilo huku akisema kwamba,hajakua na ufahamu wa masaibu ya wakaazi hao wa Parkishon. "Maneno ya maji hapo karare na sehemu zingine umeniambia sai.Baada ya ujenzi wa barabara huenda mabomba ya kupitisha maji yaliharibiwa lakini nitashiriki kikao na idara ya maji kupata suluhu kwa wakaazi eneo hilo”

Haya yanajiri wakati ambapo zaidi ya ngamia mia moja wamefariki eneo la El hadi hapa jimboni kwa madai ya kunywa maji ambayo yalikua na kemikali.

Jimbo hili linakaliwa na wafugaji,na vifo vya mifugo hao vimewasababishia hasara kubwa. Wanaitaka serikali kuwapa maji kwa dharura kuzuia maafa zaidi ya mifugo na vilevile kuhatarisha maisha ya wenyeji. Kwa niaba ya DW kutoka hapa Marsabit,Jina langu ni Michael Kwena.

Mwandishi: Michael Kwena

Mhariri: Iddi Ssessanga