1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tedros mgombea pekee WHO licha ya kupingwa na Ethiopia

Iddi Ssessanga
18 Septemba 2021

Mkuu wa shirika la afya duniani WHO, Tedros Adhanom Ghebreyesus anaonekana atakuwa mgombea pekee katika kuwania muhula wa pili wakati akijaribu kuiongoza dunia kupita katika mzozo mkubwa zaidi wa kiafaya katika karne.

https://p.dw.com/p/40U8Q
Kuwait | WHO Generaldirektor Tedros Adhanom Ghebreyesus
Picha: Jaber Abdulkhaleg /AA/picture alliance

Hasa ni namna gani atateuliwa kabla ya muda wa mwisho wa uteuzi wiki ijayo ni jambo lisilo bayana katikati mwa upinzani kutoka serikali mjini Addis Ababa, duru zimeliambia shirika la habari la Reuters.

Tedros ambaye ni waziri wa zamani wa afya wa Ethiopa anaetokea mkoa wa Tigraya, akichaguliwa kuwa mkurugenzi mkuu wa kwanza wa WHO kutoka Afrika mwaka 2017.

Soma pia: Muethiopia Tedros ndiye mkuu mpya wa WHO

Ameliongoza shirika hilo kupita milipuko kadhaa ya ugonjwa wa Ebola na pia janga laCovid-19, akinusurika ukosoaji mbaya kutoka utawala wa Trump kwa madai ya "kuipendelea China."

Wakati hajakiri hadharani kuhusu mipango yake ya kuwania tena muhula wa miaka mitano, akisema kwa amejielekeza kwenye kupambana na janga la Covid-19, vyanzo vinne vilisema ndiye mgombea pekee anaejulikana mpaka sasa.

Wapashaji habari hao walikataa kutajwa majina kutokana na usiri wa mchakato huo.

"Tedros kwa uhakika ni mgombea," kilisema chanzo kimoja kilicho na ufahamu wa moja kwa moja wa mchakato wa uchaguzi, na kuongeza kuwa kwa hatua hii hakukuwa na mgombea mbadala.

Schweiz Generaldirektor der Weltgesundheitsorganisation (WHO) Tedros Adhanom Ghebreyesus
Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus akishiriki mkutano wa Baraza la Afya Duniani kwa njia ya mtandao kutokana na janga la virusi vya corona.Picha: Christopher Black/WHO/REUTERS

Hata hivyo, Tedros - ambaye Jenerali moja wa Ethiopia amuita hadharani kuwa "mhalifu" na kumtuhumu kwa kujaribu kununua silaha kwa ajili ya vikosi vya Tigray - hatarajiwi kuteuliwa na serikali yake kama ulivyo utamaduni wa kidiplomasia, maafisa wawili wa Ethiopia waliliambia shirika la Reuters.

Soma pia: Ethiopia yamshutumu mkuu wa WHO kwa kuwasaidia waasi

Billene Seyoum, msemaji wa waziri mkuu, na Dina Mufti, msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Ethiopia, hawakupatikana kujibu maombi ya kutoa tamko.

Tedros ameilezea hali mkoani Tigray kuwa ya "kutisha" na amekuwa akitweet mara kwa mara kuhusu matukio mkoani humo lakini anakanusha kuchukua upande katika mzozo huo.

Mashauriano yanaendelea ikiwemo miongoni mwa mataifa ya Afrika kuhusu nani atapendekeza ugombea wake kabla ya tarehe ya mwisho ya Septemba 23, vyanzo vilisema.

Mchakato wa uwasilishaji rami ni wa siri na haikuwezekana kubaini iwapo uwasilishaji wa Tedros ulikuwa tayari umefanyika.

WHO haikujibu ombi la kutoa tamko. Sheria zake haziainishi kwamba mgombea laazima apendekezwe na nchi yake tu lakini kwamba tu uwasilishaji laazima ufanywe na mmoja ya mataifa wanachama wake 194.

Uteuzi rasmi unatazamiwa kufanyika Mei 2022 kwenye Baraza la Afya la Dunia.

Soma pia:WHO yasikitishwa na uamuzi wa Marekani wa kusitisha ufadhili

Mashaka ya Afrika katika kuchagua kati ya Tedros na Ethiopia

Upinzani wa Ethiopia dhidi ya Tedros unayaweka baadhi ya mataifa ya Afrika katika mashaka ya kuchagua. Taifa hilo la pili kwa wakaazi wengi barani Afrika ni gwiji la diplomasia na ndipo yalipo makao makuu ya Umoja wa Afrika. Jeshi lake linatoa walinzi wa amani nchini Sudan, Somalia na Sudan Kusini.

Tedros Adhanom Ghebreyesus, Direktor WHO
Je, Afrika itaungana kumuidhinisha Tedros kuwania muhula wa pili?Picha: Reuters/F. Coffrini

Ushawishi wake juu ya Umoja wa Afrika unamaanisha Tedros hana uwezekano wa kupata uungwaji mkono wa pamoja wa taasisi hiyo kama ilivyokuwa mara ya mwisho, lakini wanadiplomasia wanasema bado anaungwa mkono na baadhi ya mataifa ya Afrika.

"Kenya itaunga mkono uteuzi wake," Macharia Kamau, katibu mkuu wa wizara ya mambo ya nje ya Kenya, aliliambia shirika la Reuters. Alipobanwa kuhusu nani atamteua, Kamau alijibu: "Nadhani kutakuwa na kundi la mataifa."

Waziri wa nchi wa Uganda anaehusika na masuala ya nje Okello Oryem alimuita Tedros "rafiki wa siku nyingi" na kwamba Kampala ilikuwa inashauriana na serikali nyingine za Afrika Mashariki kuhusu uteuzi wake. "Endapo tutashauriana na marafiki zetu na tukabaini kuwa marafiki zetu wote wanamuunga mkono tutamuunga mkono," aliiambia Reuters.

Soma pia: WHO yaahidi tathmini huru kuhusu janga la covid-19

Tedros anaonekana kama sauti ya Afrika katika jukwaa gumu -- akitoa hoja kwa hisia kutetea upatikanaji zaidi wa chanjo za Covid-19 kwa ajili ya Afrika, na kupinga kile kinachoitwa pasipoti za chanjo, ambazo mataifa mengi ya Afrika yanahofia zitazuwia uhuru wa kusafiri wa raia wake, wanaopambana bado kupata chanjo ambazo zinapatikana kwa wingi katika mataifa ya magharibi.

Mmoja ya vyanzo vinavyofuatilia uchaguzi kilisema mataifa nje ya Afrika yatakuwa tayari kumteua Tedros, iwapo hilo litahitajika.

Chimbuko la virusi, mageuzi

Mwaka 2016-2017, Tedros alipambana dhidi ya wataalamu wengine watano wa afya wa kimataifa katika uchaguzi uliyopita wa WHO.

Uwezekano wa kuchaguliwa kwake tena ni mtihani wa shirika lake katika kushughulikia janga chini ya uongozi wake, ambao ulikosolewa vikali na rais wa zamani wa Marekani Donald Trump.

Äthiopien | PK Billene Seyoum | Sprecherin des Premierministers
Katibu wa habari wa waziri mkuu wa Ethiopia Billene Seyoum.Picha: Yohannes Geberegziabher/DW

Endapo atachuliwa tena, atasimamia hatua inafuata ya uchunguzi wa chimbuko la virusi vya corona nchini China, pamoja na uwezekano ya kulifanyia mageuzi shirika la WHO katikati mwa wasiwasi kuhusu rasilimali zake na uwezo wa kushughulikia janga la kilimwengu.

Utawala wa Trump ulimtuhumu Tedros na WHO kwa kuegemea China - madai waliokanusha - na kusitisha ufadhili wa Marekani wakati ukianzisha mchakato wa kujitoa kwenye shirika hilo.

Soma pia: WHO yaomba masoko ya wanyama hai kufungwa

Utawala wa Biden ulitangaza baada ya kuingia madarakani mwezi Januari kwamba Marekani itabakia kuwa mwanachama kutimiza wajibu wake wa kifedha huku ukifanyia kazi mageuzi.

Mageuzi hayo yanaweza kupelekea mabadiliko makubwa ndani ya shirika. Miongoni mwa mapendekezo kutoka kamati huru mwezi Mei, ni kuundwa kwa mfumo mpya wa kimataifa kuitikia haraka panapotokea mlipuko wa ugonjwa ili kusaidia kuhakikisha hakuna virusi baadae vinasababisha janga baya kama Covid-19.

Chanzo: RTRE